Halmashauri ya Mji Kasulu mkoani Kigoma, imejipanga kutekeleza uzinduzi wa miradi mbalimbali ya Serikali katika kampeni ya Mbio za Mwenge wa Taifa zinazotarajiwa kuanza itakapofika Septemba 2025 katika mkoa wa Kigoma.
Akizungumza na Buha Fm Radio leo mei 19, 2025 Baada
Kikao cha maandalizi ya Mbio za Mwenge Mratibu wa Mbio Mwenge Ndg. Daudi Stinga
amesema halmashauri ya Mji Kasulu imejipanga kufanya vizuri katika zoezi hilo
ili kuendelea kushika nafasi ya kwanza kama ilivyokuwa mwaka 2024.
“Leo tulikuwa na kikao cha maadalizi ya mwenge kwa
ajili ya halmashauri yetu ya Mji Kasulu mwaka jana tulifanya vizuri hivyo mwaka
huu tunajipanga ili tufanye vizuri zaidi kuliko mwaka jana, Mkurugenzi amekuwa
akitupa ushirikiano mzuri ndiyo maana leo tumekutana kujadili na kujipanga ili
tufanye kwa ubora zaidi” Amesema Stinga.
Aidha Stinga amesema mwaka huu watazindua miradi
mbalimbali ikiwemo miradi ya Afya, Elimu, Barabara, maji Pamoja na miradi ya
mapato ya ndani huku akiwaomba wadau kuonga mkono jitihada za serikali katika
kutekeleza miradi katika kukuza Uchumi wa nchi.
“Kwa mwaka huu tutaendelea kufuata vigezo kama
ilivyokuwa mwaka jana tutazindua miradi ya afya,elimu, Barabara, miradi ya maji
na miradi ya mapato ya ndani itakuwemo lengo kubwa tunaendelea kuangalia miongozo
inasemaje na tunaimani wananchi wataendelea kutuunga mkono ili halmashauri yetu
iendelee kufanya vizuri” Amesema Stinga.
Katika hatua nyingine Mwl. Zawadi Mnana ambaye ni mjumbe wa Mbio za Mwenge 2025 amesema mwaka huu wameanza mapema kujiandaa ili kubakia katika nafasi ya kwanza na nafasi za juu zaidi kitaifa.
“Kiukweli mwaka jana tulifanya vizuri lakini mwaka huu
tumeanza mapema mandalizi ili kuhakikisha tunakuwa nafasi za juu zaidi kitaifa
hivyo wananchi wajitokeze kwa wingi kama ilivyokuwa mwaka jana katika uwanja wa
umoja” Amesema Mwl.Mnana.
Kwa upande wake Mwl. Michael Benezeth ambaye ni
Mwenyekiti wa wakuu wa shule katika halmashauri ya Mji Kasulu amesema
maandalizi yameanza mapema ili wajumbe wapate kupendekeza maeneo ambayo
yanauhitaji ya kufikiwa na Mwenge wa kitaifa.
“Kikao cha leo kilikuwa kizuri kwa sababu wajumbe
wamepewa nafasi ya kuchagua na kupendekeza maeneo ya miradi ambayo mwenge
utaangazia na kufikiwa, lakini pia kama tutachagua miradi mizuri iliyosimamiwa
kwa ubora tutaweza kufanya vizuri na jambo la Mwenge ni la kitaifa hivyo kila
mtu ni vizuri kushiriki” Amesema Mwl.Benezeth.
Halmashauri ya Mji Kasulu kwa mwaka 2024 katika zoezi
la mbio za mwenge ilishika nafasi ya kwanza kati ya halmashauri nane za mkoa wa
Kigoma na kushika nafasi ya 40 kitaifa hivyo mwaka huu wadau wa maendeleo ya mbio
za mwenge wamejipanga kushika nafasi za juu zaidi kitaifa ili kuipa hadhi
halimashauri na mkoa kwa ujumla.
Mwandishi na Picha. Sharfati Shinji
0 Comments