Mwezi mmoja baada ya kupata ushindi wa asilimia 100 katika uchaguzi wa Wabunge, chama tawala nchini Burundi CNDD-FDD kinasherehekea miaka 20 ya kushika hatamu kikinadi mafanikio makubwa
Katika kusherehekea mafanikio hayo, Rais wa Jamhuri ya Burundi Evariste Ndayishimiye ameongoza maelfu ya wafuasi wa Chama Tawala nchini humo CNDD - FDD, kutafakari na kujadili wapi walitoka, waliko na waendako tangu Chama hicho kilipokomboa taifa la Burundi kutoka katika machafuko ya vita.
Akihutubia katika kongamano maalum katika chuo kukuu cha Ufundi, sayansi na teknolojia makao makuu ya Nchi ya Burundi mkoani Gitega, Rais Ndayishimiye amesisitiza warundi kuendelea kuwa na umoja na mshikamano,
Amebainisha kuwa kabla ya CNDD-FDD kushika hatamu mwaka 2005 Burundi ilikuwa imegawanyika vipandevipande hasa ukabila, chuki za kisiasa, ubaguzi wa maeneo na vitendo vya uhalifu kukithiri na amewahimiza Warundia kuondoa matabaka baina yao.
"Nchi yetu nzuri ilikuwa shimoni, kulikuwa na uhalifu mwingi, ukabila, ukanda, chuki za kisiasa na umasikini wa kupindukia, tangu tulipoingia madarakani baada ya mapambano, nchi hii sasa iko vizuri" Amesema Rais Ndayishimiye
Ameweka bayana kuwa kilichowapeleka vijana msituni na kutumia mitutu ya Bunduki kwa sasa hakipo na Burundi ni moja, warundi ni wamoja na uchumi umeanza kuimarika.
Awali Katibu mkuu wa chama hicho Reverien Ndikuriyo akimkaribisha Rais Ndayishimiye kufungua kongamano alibainisha kuwa Chama cha CNDD-FDD kimefanya kazi kubwa ya kurejesha heshima ya Warundi ndani na nje ya nchi
Amesisitiza kuwa viongozi na raia wote wameendelea kusikiliza na kuzingatia mafundisho ya chama hasa katika kuongeza juhudi katika kufanyakazi hasa katika sekta ya kilimo, biashara na uchimbaji wa madini ili kuongeza kipato kwa jamii na Taifa.
Baadhi ya viongozi waandamizi wa chama cha CNDD-FDD wakimlaki Rais Ndayishimiye
Mh. Reverian Ndukuliyo, Amepongeza serikali kwa kusimamia misingi ya utawala bora na kuhakikisha amani na utulivu kwa jamii hali inayochangia kasi ya maendeleo nchini Burundi
0 Comments