Siku ya wakimbizi 2025 yaadhimishwa kwa shukurani

 
Dunia leo inaadhimisha siku ya wakimbizi kimataifa huku kukiwa na wimbi jipya la wakimbizi wapya katika maeneo mbalimbali kutokana na kuwepo kwa mapigano katika nchi ya DRC, na nchi za Mashariki ya Kati hususani Israel, Palestina, Yemen, Ukraine, Urusi na Irani.

Tanzania ni miongoni mwa mataifa yanayohifadhi wakimbizi wa zamani wa DRC na Burundi na kundi jipya la wakimbizi kutoka Mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo.

Tofauti na miaka ya nyuma ambapo maadhimisho ya siku ya wakimbizi duniani yaligubikwa na malalamiko mengi, mwaka huu wakimbizi, UHNCR na jamii wameungana kushukuru namna Tanzania na watanzania wanavyovumiliana na kushirikiana katika kuhakikisha kunakuwepo na mahusiano mazuri, utu, amani na mshikamano miongoni mwa raia na wakimbizi.

Akihutubia katika mkutano mkubwa wa wakimbizi mapema leo katika kambi ya Nyarugusu inayohifadhi Raia wa Burundi pamoja na DRC, Mkuu wa ofisi ys UNHCR Bw. Jean Bosco Ngomoni ameishukuru Tanzania na raia wake kwa kuonesha mshikamano thabiti kwa wakimbizi.

Bw. Ngomoni amesema hatua mbalimbali za utoaji wa huduma zinaendelea kutekelezwa sambamba na kuhakikisha kuna amani ya kudumu katika nchi walizotoka na akasisitiza kuwa nchi ya Burundi sasa ina amani na usalama wa uhakika unaowezesha wakimbizi kurejea nchini mwao kwa hiari ili wakaijenge nchi yao tofauti na DRC ambako hali bado haijaimarika.

Jean Bosco Ngomoni mkuu wa Ofisi ya UNHCR Kasulu mkoani Kigoma inayotoa huduma kwa wakimbizi katika Kambi ya Nyarugusu yenye wakimbizi kutoka Burundi na DRC 

Mkuu huyo wa UNHCR Kasulu amesisitiza kuwa kutokana na mshikamano wa pamoja na serikali na umoja wa mataifa, Tanzania imeendelea kupokea wakimbizi wapya na kwamba mwaka 2023 wakimbizi takribani 14,000 waliingia nchini humo na wengine 3000 wamepokelewa mwaka huu wakitokea nchi ya Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo na kwamba serikali ya Tanzania imekuwa mstari wa mbele kuhudumia wakimbizi wanaoingia nchini na kusisitiza kuwa wakimbizi watakakaofanya maamuzi ya kurejea nchini mwao watakuwa wamefanya maamuzi sahihi.

Wakimbizi wenyewe wana maoni gani kuhusu siku ya mkimbizi duniani? Hawa hapa ni baadhi ya waliozungumza na vyombo vya habari na kukiri kuwa Tanzania imekuwa sehemu ya msaada kwa usalama wa maisha yao, na kupongeza serikali inayoshirikiana na Umoja wa Mataifa kutoa huduma kwa wakimbizi ingawa kwa sasa wanakabiliwa na changamoto ya upungufu wa misaada hususani chakula. Ilakoze Lyidia, ni mama mkimbizi kutoka nchi ya Burundi mwenye

Naye Amrani Juma, kutoka nchi ya DRC ambaye yupo kambini tangu mwaka 1998 anakiri kuwa kuna hali mbaya ya uchumi inayoikumba dunia kutokana vita vinavyoendelea imekuwa kikwazo kwa upatikanaji wa huduma muhimu zikiwemo za afya na elimu.

Baadhi ya wakimbizi waliohudhuria maadhimisho ya siku ya wakimbizi duniani katika Kambi ya Nyarugusu wilayani Kasulu

Kwa upande wake mwenyekiti wa kambi kambi ya Nyarugusu Bw. Manilakiza Japhet, alisema bado zipo changamoto zinazowakabili wakambizi wanaoishi kambini na kuomba UNHCR kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania na mataifa yanayotoa huduma kambini humo kutafuta hifadhi za kudumu kwaajili ya wakimbizi hao pamoja na nchi ya Tanzania kutoa hifadhi ya kudumu.

Misimamo ya Rais wa Marekani Donald Trump kuhusu wahamiaji, nayo imegusa siku ya wakimbizi ambapo pamoja na kulaumiwa kwa kuzuia fursa kwa wakimbizi kupata hifadhi nchi ya tatu, jumuiya ya wakimbizi nchini Tanzania inauomba umoja wa mataifa kutafuta nchi nyingine tofauti na Marekani kama anavyosisitiza Mwenyekiti wa kambi

Ndugu SIasa Manjenje mkuu wa kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu iliyopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma

Wakati huo huo Wakimbizi katika kambi ya Nyarugusu iliyopo wilayani Kasulu mkoani Kigoma wametakiwa kuwalea watoto katika maadili yanayofaa ili kizazi chao kiweze kumaliza tatizo la ukimbizi linalozikumba baadhi ya nchi za maziwa makuu.

Akizungumza katika maadhimisho hayo Mkuu wa kambi ya Nyarugusu Bw. Siasa Majenje amesema kutokuwa na malezi bora kumetajwa kuwa tishio kwa vizazi vilivyopita na vilivyopo na kusisitiza malezi bora kuwa ni suluhu la kudumu kwa ukimbizi.

"Vurugu zinazotokana na vita katika maziwa makuu zimekuwa zikizalisha wakimbizi wengi ambapo wanaoteseka zaidi ni watoto, naomba muwalinde na kuwalea watoto wenu vizuri ili kuokoa maisha yao, huenda kesho wakawa sababu ya kusitisha mapigano" Anasema Majenje

Mkuu huyo wa kambi alisema vurugu nyingi zinasababishwa na madhaifu ya kibinadamu ya kutamani mali na madaraka na kwamba hali hiyo inaweza kubadilika kwa kupanda mbegu za amani kwa watoto ili watakapokua wasifanye makosa kama waliyoyafanya wazazi wao.

Kuhusu maombi yaliyowasilishwa na wakimbizi, Mkuu huyo wa kambi ambaye ndiye aliyekuwa mgeni rasmi ameahidi kuyawasilisha kwa mamlaka zinazohusika ili yafanyiwe kazi na kutafutiwa ufumbuzi

Tazama Video namna wakimbizi walivyoonesha vipaji vya hali ya juu katika michezo mbalimbali kwa kubofya link hii https://www.youtube.com/shorts/gI2DhW-FyVo?feature=share 

Pamoja na hotuba, ngoma na burudani nyingine kumefanyika mchezo wa kirafiki wa mpira wa miguu uliokutanisha timu ya wakimbizi na timu ya raia kutoka Makere halmashauri ya wilaya ya Kasulu

Katika mchezo huo wa ujirani mwema, kikosi cha wakimbizi kimeondoka kifua mbele kwa ushindi wa magoli matatu (3) kwa nunge shidi ya Makere FM

Mkuu wa Kambi Bw. Siasa Manjenje akikabidhi Kombe kwa timu ya wakimbizi iliyotwaa ubingwa wa siku ya mkimbizi duniani 2025 katika kambi ya Nyarugusu

Mshindi wa kwanza amekabidhiwa kombe pamoja na mbuzi watatu (3) wakati Makere FC ikipata zawadi ya Mbuzi wawili (2).

Akikabidhi zawadi hizo Mkuu wa Kambi hiyo Bw. Manjenje amewapongeza kwa mchezo mzuri unaodhihirisha ujirani mwema baina ya Wakimbizi na Wenyeji.

Timu ya mpira wa miguu ya Wakimbizi wa Nyarugusu inayojumuisha raia wa Burundi na DRC ikipokea zawadi zake kutoka kwa mgeni rasmi mkuu wa Kambi hiyo

Timu ya soka ya Makere FC ambayo imepata tuzo ya mbuzi wawili baada ya kuibuka mshindi wa pili katika fainali za siku ya wakimbizi duniani 2025 katika mtangange uliopigwa ndani ya kambi ya wakimbizi Nyarugusu kama sehemu ya ujirani mwema.

Tanzania inahifadhi wakimbizi zaidi ya 150,000 wengi wao wakitokea nchini DRC na Burundi waliokimbia machafuko katika nchi zao na kupata hifadhi katika kambi za Nduta wilayani Kibondo na Nyarugusu wilayani Kasulu.


Post a Comment

0 Comments